MWANAMKE MAKINI BLOG

Advertise Here

Saturday 8 November 2014

BUNGE KUMPONGEZA SPIKA MAKINDA KWA USHINDI SADC-PF



WABUNGE wa bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wameridhia azimio la kumpongeza spika wa bunge hilo mheshimiwa ANNE MAKINDA kwa kuchaguliwa kuwa rais wa Jukwaa la Mabunge ya Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC-PF).

Akisoma azimio hilo  bungeni mjini Dodoma mwenyekiti wa kamati ya mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa mheshimiwa MUSSA ZUNGU amemzungumzia mheshimiwa MAKINDA kuwa ni mzoefu wa kutosha katika medani za siasa na uongozi kwa zaidi ya miaka 37 kwa kushika nyadhifa mbalimbali kitaifa na kimataifa.

Amesema kutokana na jitihada mbalimbali zinazofanywa na rais JAKAYA KIKWETE za kuitangaza nchi ya Tanzania zilisaidia sana katika mchakato wa kumnadi mheshimiwa MAKINDA kwa wajumbe wa mkutano na kufanikiwa kushinda kwa kishindo bila ya kupingwa.

Wakiunga mkono azimio hilo baadhi ya wabunge waliochangia wamempongeza mheshimiwa MAKINDA na kusema ni mtu anayestahili kupata nafasi hiyo kutokana na uchapakazi wake.

Mbunge wa Kigoma Kaskazini mheshimiwa ZITTO KABWE amesema kwa mara nyingine tena Tanzania imeshamiri katika medani ya dunia kitu ambacho kinaleta heshima kubwa na ni ishara ya mafanikio makubwa ya kidiplomasia katika nyanja ya kimataifa.

Amesema kupata kwake nafasi hiyo kunaonyesha wazi kuwa ni jinsi gani bunge la Jamhuri lilivyokuwa halikufanya makosa kumchagua kuwa spika  na kusema ana aamini atapeperusha bendera ya Tanzania vizuri anakokwenda na kuwataka wabunge kumuunga mkono kwa kuwa ni mtu mzuri.

Kwa upande wake mbunge wa viti maalum mheshimiwa BERNADETA MUSHASHU ameungana na wengine kumpongeza na kusema hawakukosea kumchagua kwa kuwa sifa anazo kutokana na kuandaliwa na Taifa hili na kumuomba mungu ampe uwezo mkubwa wa kupeperusha bendera ya Tanzania.

Mbunge wa viti maalum mheshimiwa RUKIA AHMED amesema anaona fahari kutokana na ushindi huo na kwamba uteuzi huu haujaja bure bali umekuja kutokana na juhudi kubwa alizonazo katika utendaji kazi wake wa kutobagua dini,kabila wala vyama vya siasa.

Wakati huo huo mheshimiwa MAKINDA  amewataka wabunge wa vyama vyote vya siasa kuamka na kubadilisha fikra zao ili wafikirie Maendeleo.

Mheshimiwa MAKINDA akitoa shukrani kwa wabunge  amesema  Maendeleo sio Taifa bali yanapaswa kuanzia kwa wabunge wenyewe kwa kuwa   hivi sasa nchi nyingi duniani wanachosimamia ni suala la uchumi na upo uwezekano wa Tanzania kama wasiposimamia msingi huo ikabaki nyuma.

Amewataka kuamka na kusimamia suala hilo ingawa mwaka huu ni mgumu kwa sababu wanaelekea kwenye uchaguzi lakini isiwe sababu ya kuacha kufanya kazi na kuanza kupigana vijembe.

No comments:

Post a Comment